Saturday, December 12, 2015

KUAPISHWA KWA BARAZA LA MAWAZIRI NA HM. MAGUFULI

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Magufuli akimuapisha Ummy Ally Mwalimu kuwa Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto.
Rais wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania Dk. John Pombe Magufuli akimuapisha Mh. Nape Nnauye kuwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Wasanii na Michezo Ikulu.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli akimuapisha Jenista Joakim Mhagama kuwa Waziri wa Nchi , Ofisi ya Waziri Mkuu Ikulu jijini Dar es Salaam.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimuapisha Dk. Abdallah Saleh Possi kuwa Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Wenye ulemavu) Ikulu jijini Dar es Salaam.
Mh, Rais Dk. John Pombe Magufuli akimuapisha Mwigulu Lameck Nchemba kuwa Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi Ikulu jijini Dar es Salaam.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli akimkabidhi  Muongozo wa kufanyia kazi  kwa Waziri wa Katiba na Sheria Dkt Harrison George  Mwakyembe mara baada ya kumuapisha Ikulu jijini Dar es Salaam.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli akimuapisha Profesa Sospeter Mwijarubi Muhongo kuwa Waziri wa Nishati na Madini Ikulu jijini Dar es Salaam.

Rais wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania Dk. John Pombe Magufuli katika picha ya pamoja na Mawaziri wake mara baada ya kuwaapisha Jijini Ikulu Dar es salaam.

Thursday, December 10, 2015

MHE.RAIS JOHN MAGUFULI ATANGAZA BARAZA LA MAWAZIRI



Rais John Magufuli akitangaza baraza la mawaziri Ikulu jijini Dar es salaam, Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan na kushoto ni Waziri Mkuu Mhe Majaliwa Kassim Majaliwa.

BARAZA LA MAWAZIRI TANZANIA

Wizara ya Ofisi ya Rais,Tamisemi, Utumishi na Utawala Bora.
  • Mawaziri - George Simbachakene na Angella Kairuki
  • Naibu Waziri - Sumeilam Jafo. Naibu.
Wizara ya Ofisi ya Makamu wa Raisi, Muungano na Mazingira
  • Waziri - January Makamba
  • Naibu Waziri – Luhaga Jerrson Mpina
Ofisi ya Waziri Mkuu: Sera, Bunge, Kazi Vijana, Ajira na Walemavu
  • Waziri - Jenista Muhagama
  • MaNaibu – Dkt. Possy Abdallah na Anthony Mavunde.
Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
  • Waziri - Mwigulu Nchemba
  • Naibu Waziri - William Ole Nasha
Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.
  • Waziri Bado hajapatikana.
  • Naibu Waziri – Inj. Edwin Ambandusi Ngonyani
Wizara ya Fedha na Mipango
  • Waziri Bado hajapatikana.
  • Naibu Waziri - Ashantu Kizachi
Wizara ya Nishati na Madini
  • Waziri - Prof. Mwigalumi Muhongo.
  • Naibu Waziri - Medalled Karemaligo.
Wizara ya Katiba na Sheria
  • Waziri - Harrison Mwakyembe
Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afika Mashariki, Kikanda na Kimataifa.
  • Waziri - Dk. Augustino Mahiga
  • Naibu Waziri – Dkt. Susan Kolimba.
Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
  • Waziri - Dk. Hussein Mwinyi
Wizara ya Mambo ya Ndani
  • Waziri - Charles Kitwanga.
Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi.
  • Waziri - William Lukuvi
  • Naibu Waziri - Angelina Mabula
Wizara ya Maliasili na Utalii
  • Waziri Bado hajapatikana.
  • Naibu Waziri– Inj. Ramol Makani
Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji.
  • Waziri Charles Mwijage.
Wizara ya Elimu,Sayansi Teknolojia na Ufundi.
  • Waziri Bado hajapatikana.
  • Naibu Waziri – Inj. Stella Manyanya
Wizara ya Afya,Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
  • Waziri - Ummy Mwalim
  • Naibu Waziri – Dkt. Hamis Kigwangala
Wizara ya Habari, Utamaduni, Wasanii na Michezo
  • Waziri - Nape Nnauye
  • Naibu Waziri - Anastasia Wambura.
Wizara ya Maji na Umwagiliaji
  • Waziri – Prof. Makame Mbarawa
  • Naibu Waziri– Inj. Isack Kamwela 

Mh.Rais John Pombe Magufuli katika picha ya pamoja na wanahabari waliofika kumsikiliza wakati akitangaza baraza la mawaziri Ikulu jijini Dar es salaam. Makamu wa rais Samia Suluhu Hassan na kushoto ni Waziri Mkuu Mhe Majaliwa Kassim Majaliwa.

Wednesday, December 9, 2015

MH, RAIS JOHN MAGUFULI AFANYA USAFI UFUKWE WA FERRY.





Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John P. Magufuli akiwa pamoja na Mke wake Mama Janeth Magufu katika  eneo la ufukwe wa ferry jijini Dar es Salaam.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akizoa taka katika  eneo la ufukwe wa ferry jijini Dar es Salaam.

Thursday, December 3, 2015

MH.RAIS MAGUFULI NA VIONGOZI WA UMOJA WA SEKTA BINAFSI.


Rais wa Jamhuri ya Muungano Tanzania Dkt.John Pombe Magufuli amewapa siku saba kuanzia tarehe 03/12/2015 wafanyabiashara wote ambao waliingiza mizigo yao bila kulipa kodi wakalipe kwani baada ya hapo watachukuliwa hatua kali za kisheria.

Hayo yamesemwa leo Ikulu jijini Dar es Salaam na Mheshimiwa Rais katika mkutano wake na wadau wa sekta binafsi alipoamua kufanya mazungumzo nao pamoja na kuwasikiliza maoni yao ikiwa ni sehemu ya ahadi zake katika kipindi cha kampeni za kuomba kura za kiti cha Urais,lengo likiwa ni kukuza uchumi wa nchi kupitia sekta binafsi.

Mheshimiwa Rais aliendelea kusema kuwa katika kipindi hichi cha miaka mitano amedhamiria kuijenga nchi na watu wasimuelewe vibaya kwa maamuzi anayofanya kwani ni kwania njema ya kuleta maendeleo na siyo ujeuri.

“Tutaangalia namna ya kupunguza utitiri wa ushuru katika bidhaa mbalimbali,mfano katika kipindi cha kampeni niligundua katika Mkoa wa Kagera na Kilimanjaro wanakolima zao la Kahawa,wamekuwa wakitozwa tozo 26 kwa zao hilo na hiyo imechangia kusababisha wafanyabiashara wa zao hilo kufanya biashara haramu ya kupeleka zao hilo kwa magendo kuuza katika nchi jirani”,alisema Mheshiwa Rais Dkt. Magufuli.

Pamoja na hayo Mheshimiwa Dkt.Magufuli amewaahidi wadau wasekta binafsi ushirikiano mkubwa kwani anatambua mchango wao katika kukuza uchumi na pia amewataka wadau hao kuwa wazalendo na kuliacha kukwepa kulipa kodi ili tuweze kujenga taifa lenye maendeleo makubwa ya kiuchumi.

Mheshimiwa Rais Dkt.Magufuli ameendelea kusema kuwa kama kutakuwa na mfayabiashara yeyote atakayetaka kuwekeza na akakwamishwa na mtu aliyechini ya uteuzi wake basi mtu huyo ataondoka kwani sasa ni wakati wa wadau wa sekta binafsi kuanza kuanzisha viwanda mbalimbali vitakavyo toa ajira.

Pamoja na hayo Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli amewapa mawazo ya kibiashara wadau wa sekta binafsi kuanzisha kampuni ya kutenganisha udongo unaotoka kwenye machimbo ya madini,kuanzisha viwanda vya samaki pembezoni mwa bahari pamoja na kutengeneza samani zitokanazo na mazao ya misitu.

Kwa upande wa Mwenyekiti wa Taasisi ya Sekta Binafsi (TPSF) Bw.Regnald Mengi amesema kuwa wako tayari kumpa ushirikiano mkubwa Mheshimiwa Rais katika kuhakikisha uchumi watanzania unakuwa kwa haraka na pia amemuomba mheshimiwa rais kuendelea kukemea masuala ya rushwa pamoja kusaidia kupunguza utitiri wa kodi.

HOTUBA YA RAIS DK.JOHN P. MAGUFULI



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh, Dk. John Pombe Magufuli akiongea na Viongozi na Wawakilishi wa Umoja wa Sekta Binafsi nchini.

ZIARA YA KUSHTUKIZA BANDARINI NA TRL ALIYOIFANYA MH. MAJALIWA

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akimwonyesha Kaimu Meneja wa Bandari ya Dar es salaam, Bw. Abel Mhanga orodha ya makontena 2,431 yaliyopitia kwenye banda ya Dar es salaam bila kulipiwa kodi bandarini Desemba 3, 2015.

*Akuta makontena 2,431 yametoka bila kulipiwa ushuru
*Ataka majina yaletwe ofisini leo saa 11 jioni
*Atoa wiki wiki moja kwa mfumo wa malipo kubadilishwa
*Akagua mabehewa, awaweka kiporo TRL

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amefanya ziara nyingine ya kushtukiza bandarini na kukagua mfumo wa upokeaji na utoaji mizigo na utozaji wa malipo baada ya kupewa taarifa kwamba kuna makontena 2,431 yametolewa bila kulipiwa ushuru.

Waziri Mkuu alisema kwa mujibu wa taarifa ya ukaguzi wa bandari ya kuanzia Machi hadi Septemba 2014, makontena hayo yalipita bila kulipiwa kodi kupitia bandari kavu nne (ICDs) ambazo ni JEFAG, DICD, PMM na AZAM.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, ni watumishi 10 tu ambao wamesimamishwa kazi kutokana na makosa hayo. “Mmeamua kuwasimamisha kazi watu wadogo na kuwaacha wakubwa wanaendelea na kazi. Hatuwezi kuendelea kuikosesha Serikali mapato namna hii,” alisema Waziri Mkuu.

Waziri Mkuu amemtaka Kaimu Meneja wa Bandari, Bw. Hebel Mhanga amletee ofisini majina ya watumishi wote waliohusika na ukwepaji kodi huo ifikapo leo saa 11 jioni. Pia amempa Meneja huyo wiki moja kuhakikisha kuwa mamlaka hiyo inabadilisha mfumo wa utozaji malipo kutoka kwenye billing system na badala yake kuweka mfumo wa malipo wa kielektroniki (e-payment).

Ametoa agizo hilo leo (Alhamisi, Desemba 3, 2015), wakati akikagua idara mbalimbali za mamlaka ya bandari na kuona ukaguzi wa mizigo unavyofanyika kwa kutumia scanners. Akiwa kwenye chumba cha scanner mojawapo, Waziri Mkuu alikuta manifest moja ikisema kontena limejaa diapers lakini picha ya kwenye kompyuta ya scanner ilionyesha kuwa ndani ya kontena hilo kuna vitu kama vifaa vya umeme.

Kwa mujibu wa Kaimu Meneja Bandari upande wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Bw. Ben Usaje ambaye pia ni msimamizi wa kitengo cha scanner, inapobainika taarifa kama hiyo inapaswa itumwe kwa wenye ICDs ili wafanye ukaguzi kwa kulifungua kontena ili kuhakikisha mali zilizomo ndizo zilizoandikishwa kwenye manifest.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu Majaliwa amefanya ziara ya kushtukiza kwenye ofisi za Shirika la Reli (TRL) na kukagua mabehewa yaliyokuwepo kisha akazungumza na baadhi ya wafanyakazi waliokuwepo kwenye stesheni hiyo ambako alibaini madudu kwenye malipo ya mishahara na makato ya michango ya wafanyakazi.

Akizungumza na Mkurugenzi Mkuu TRL, Mhandisi Elias Mshana, Waziri Mkuu alisema amefika kwenye shirika hilo ili kujifunza utendaji wao kazi lakini anazo taarifa za wao kupewa fedha na Serikali kiasi cha sh. bilioni 13.5/- ili waendeleze miundombinu ya reli lakini hawakufanya hivyo. “Nia ya kuwapa fedha hizo ilikuwa ni kuboresha miradi ili muweze kujiendesha kibiashara lakini nyie mkaamua kujilipa wenyewe,” alisema.

“Ninazo taarifa kuwa baada ya hapo, mlikopa sh. bilioni 3 kutoka benki ya TIB ili kuendesha miradi ya shirika lakini badala ya kufanya miradi, fedha hizo mkaamua nazo kujilipa mishahara. Sasa sijui mnarudishaje huo mkopo wakati hakuna mradi wowote uliofanyika,” alihoji bila kupata majibu.

Alipoulizwa wafanyakazi wana matatizo gani hapo TRL, Katibu wa TRAWU, Bw. Boaz Nyakeke alisema wanadai malimbikizo ya makato yao kwenye mifuko ya pensheni, malimbikizo ya makato kwenye SACCOS na malimbikizo ya kuanzia Julai – Novemba 2014.

Waziri Mkuu kwa upande wake alimtaka Mhandisi Mshana asimamie uboreshaji huduma za usafiri wa treni katika Jiji la Dar es Salaam ili hata mabasi ya mwendo kasi yatakapoanza wananchi waweze kuwa na uhuru wa kuchagua aina ya usafiri wautakao.

“Tunataka kujenga yadi kubwa nje ya mji ili watu wenye magari wawe wanayaacha huko na kutumia usafiri wa treni au DART kuja mjini kama njia mojawapo ya kupunguza msongamano wa magari jijini Dar es Salaam,” alisema.

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
2 MTAA WA MAGOGONI,
S. L. P. 3021,
11410 DAR ES SALAAM
ALHAMISI, DESEMBA 3, 2015.

Mh.Kassim Majaliwa akipata maelezo kuhusu utoaji bili za kulipia kodi za serikali kwa watumiaji wa bandari ya Dar es salaam kutoka kwa ofisa mwandamizi wa masuala ya fedha, Bw. Sartho Mbuya wakati alipotembelea bandari hiyo Desemba 3, 2015 kutaka kujua ukweli wa tuhuma za makontena 2,431 yaliyopita bandarini hapo bila kulipiwa kodi za serikali.
Waziri Mkuu,Kassim Majaliwa akitembelea stesheni ya reli ya Dar es Salaam Desemba 3, 2015.

Friday, November 27, 2015

WAZIRI MKUU AFANYA ZIARA YA KUSHTUKIZA TRA

Waziri Mkuu Mhe Majaliwa Kassim Majaliwa leo ameamuru kukamatwa kwa maafisa kadhaa wa Mamlaka ya Mapato (TRA) na wengine kufukuzwa kazi baada ya kufanya ziara ya kushtukiza Bandarini na kukuta madudu ambayo hakuyafurahia.

Maafisa hao, ambao kwa sasa tunahifadhi majina ili Jeshi la Polisi liweze kuwashughulikia, wametakiwa pia kusalimisha hati zao za usafiri.

Hii imekuja baada ya kugundulika kwamba kuna makontena 349 yenye thamani ya zaidi ya bilioni 80 ambayo data za Mamlaka ya Bandari inazo lakini katika mtandao wa TRA hayaonekani.
Majaliwa Kassim Majaliwa  akimkabidhi Kamishina Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Rished Bade orodha ya makontena  349. yenye kodi ya serikali ya thamani ya  shilingi bilioni 800 yalitoka kwenye bandari ya Dar es salaam bila kulipiwa kodi.
Waziri Mkuu Mhe Majaliwa Kassim Majaliwa akimwonyesha orodha ya makontena 349 yaliyopotea yenye thamani ya shilingi bilioni 80 na TRA haina taarifa.
Waziri Mkuu Mhe Majaliwa Kassim Majaliwa akiagana na viongozi wa TRA na TPA.

WAZIRI MKUU AWABANA UPOTEVU WA MAKONTENA 349, YENYE THAMANI YA TSH. BILIONI 80/=

WAZIRI MKUU Majaliwa Kassim Majaliwa amewasimamisha kazi maafisa watano na watumishi watatu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kutokana na upotevu wa makontena 349 yenye thamani ya zaidi ya sh. bilioni 80/-.
Akizungumza na viongozi wa Mamlaka ya Bandari pamoja na viongozi wa TRA katika ziara ya kushtukiza leo mchana (Ijumaa, Novemba 27, 2015), Waziri Mkuu amewataka Kamishna Mkuu wa TRA, Bw. Rished Bade na Naibu Kamishna Mkuu wa TRA, Bw. Lusekelo Mwaseba wahahakikishe wanashirikiana na polisi kufuatilia upotevu huo na kwamba fedha hizo zinapatikana na zinarudi Serikalini.

Akitangaza uamuzi huo baada ya kufanya kikao na baadhi ya viongozi wa Serikali bandarini hapo, Waziri Mkuu aliwataja maafisa waliosimamishwa kazi kuwa ni Kamishna wa Forodha, Bw. Tiagi Masamaki na Mkuu wa Kituo cha Huduma kwa Wateja, Bw. Habibu Mponezya.

“Hawa wanasimamishwa kazi. IGP ninaagiza hawa watu wakamatwe na kuisaidia polisi. Hati zao za kusafiria zikamatwe na mali zao zikaguliwe kama zinaendana na utumishi wa umma,” alisema Waziri Mkuu.

Maafisa wengine waliosimamishwa kazi ni Mkuu wa kitengo cha TEHAMA, Bw. Haruni Mpande, Bw. Hamisi Ali Omari (hakutaja ni wa idara gani), na Mkuu wa Kitengo cha Bandari Kavu (ICD In-Charge), Bw. Eliachi Mrema. “Hawa wanasimamishwa kazi hadi uchunguzi utakapokamilika na pia wawe mikononi mwa polisi,” alisema.

Pia aliagiza watumishi watatu wa mamlaka hiyo wahamishwe kutoka Dar es Salaam na kupelekwa mikoani. Watumishi hao ni Bw. Anangisye Mtafya, Bw. Nsajigwa Mwandengele na Bw. Robert Nyoni.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amemwagiza Katibu Mkuu wa Hazina, Dk. Servacius Likwelile ambaye alikuwepo kwenye kikao hicho, kuhakikisha kuwa anapeleka wataalamu kutoka Wakala wa Serikali Mtandao (e-Govt) haraka iwezekanavyo ili wakakague mifumo ya taarifa na kubaini jinsi ambavyo wizi huo unafanyika.

“Ninataka uchunguzi uanze kufanyika mara moja, tafuteni njia ambazo zinatumika kama mianya ya wizi kutokea hapa bandarini hadi kwenye ICDs. Nataka hayo makontena yatafutwe hadi yajulikane yako wapi, na fedha hiyo ihakikishwe inarudi serikalini,” alisema.

Kikao hicho kilihudhuriwa pia na Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, Bw. Ernest Mangu, Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Dkt. Florens Turuka, Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Dkt. Shaaban Mwinjaka, Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya DSM, Suleiman Kova, Mkurugenzi wa Mamlaka ya Bandari (TPA), Bw. Awadh Massawe na viongozi mbalimbali kutoka TRA na TPA.

Mapema akijibu maswali ya Waziri Mkuu, Kamishna Mkuu wa TRA, Bw. Bade alikiri kwamba kuna upotevu wa makontena ambao huwa unafanyika kati ya bandarini na ICDs na hasa ICD ya Ubungo. Akitoa ufafanuzi, alisema kwamba walifanya ukaguzi kwenye ICD moja na kukuta makontena 54 yamepotea kwa njia za wizi.

“Hata hivyo, tulipoendelea na ukaguzi, namba iliongezeka na kufikia 327. Tunaendelea kufuatilia kwa kushirikiana na TAKUKURU. Mmiliki wa ICD ametakiwa kulipa faini sh. bilioni 12.6/- na ameshalipa sh. bilioni 2.4/-,” alifafanua.

Alipoulizwa na Waziri Mkuu kama ana majina ya watumishi wanaohusika na wizi huo, Bw. Bade akakiri kwamba anayo lakini siyo kwa wakati huo labda ayapate kutoka kwa wasaidizi wake. Ndipo Waziri Mkuu akamuonyesha orodha ya makontena 349 yenye taarifa zote hadi namba za magari yaliyobeba mizigo hiyo na Bw. Bade akakiri kwamba orodha hiyo ni ya kweli.

“Kwa utaratibu huo hatuwezi kufika, labda baadhi ya watu waondolewe kazini”. Ndipo akaanza kutaja majina ya maafisa hao waliosimamishwa kazi.



IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
2 MTAA WA MAGOGONI,
S. L. P. 3021,
11410 DAR ES SALAAM
IJUMAA, NOVEMBA 27, 2015.


Wednesday, November 25, 2015

JUKWAA HURU LA WAZALENDO KWA RAIS DK. JOHN MAGUFULI.


Mwenyekiti wa Jukwaa Ally Salum akizungumza na Waandishi wa habari leo katika hoteli ya Travertine, Magomeni jijini Dar es Salaam (kulia)  Katibu wake, Mtela Mwampamba.

JUKWAA HURU LA WAZALENDO

TAMKO LA JUKWAA KWA VYOMBO VYA HABARI
 
Ndugu Wanahabari,

Mbele yenu sisi tuliowaita hapa ni Jukwaa Huru la Wazalendo ambalo limeitisha mkutano huu ili kufikisha yale tuliyoyakusudia kuwaeleza umma wa watanzania.

Sote tunatambua kuwa nchi yetu imetoka katika uchaguzi mkuu ambao umetupatia viongozi wapya wa awamu ya tano ya uongozi wa taifa letu chini ya Dr. John Pombe Joseph Magufuli. Tunapenda kuwapongeza watanzania wote kwa uchaguzi wa amani na utulivu. Aidha kwakua ndio mara yetu ya kwanza kuzungumza nanyi tunapenda kuwapongeza wanahabari wote kwa kazi nzuri ambayo mmekua mkiifanya kabla, wakati na baada ya uchaguzi mkuu nchini. Tunawashukuru sana.

Mkutano wetu huu umebeba madhumuni makubwa mawili.
Kwanza ni kumpongeza Mh. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa hotuba yake aliyoitoa Bungeni siku ya ufunguzi wa Bunge la 11 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mnamo tarehe 19/11/2015. Tunaiunga mkono Hotuba yake ambayo kwa kweli ilikuwa imebeba Uzalendo, Ujasiri, dira ya kweli ya maendeleo ya taifa letu na muuelekeo mpya wa Serikali ya awamu ya tano. Mambo yote aliyozungumzia Mh. Rais yamebeba maslahi mapana ya nchi yetu na yanalenga kuijenga Tanzania mpya ambayo waasisi wa Taifa letu Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Abeid Amani Karume walikusudia kuijenga.

Pili, pamoja na mambo mengi yaliyogusiwa na hotuba ya Mh. Rais, eneo la kubana matumizi na kupunguza matumizi yasiyo ya lazima kwa Serikali ni moja katika mambo ambayo Jukwaa hili limeamua kuyaunga mkono kwa vitendo. Mh. Rais alitoa mchanganuo wa eneo moja tu la safari za nje na jinsi lilivyo ligharimu Taifa mabilioni ya shilingi na kuahidi kuwa serikali ya awamu ya tano chini ya uongozi wake itajikita katika kupunguza matumizi yasiyo ya lazima.

Aidha Mh. Rais ameanza kutekeleza kwa vitendo ahadi yake hiyo ya kupunguza matumizi yote yasiyo ya lazima Serikalini, ikiwemo hafla, warsha, makongamano na safari za nje.

Jukwaa Huru la Wazalendo, linatambua kuwa kwa miaka kadhaa mbunge wa Kigoma Mjini Mh. Zitto Kabwe amekuwa na msimamo wa kutokupokea posho za kitako tangu akiwa mbunge wa Kigoma Kaskazini katika Bunge la 10. Pamoja na Mh. Zitto, Jukwaa pia limepokea taarifa za baadhi ya wabunge wa Bunge la 11 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania walioamua kuunga mkono juhudi za Mh. Rais za kupunguza matumizi yasiyo ya lazima serikalini kwa kukataa hadharani kupokea posho ya kitako ya mbunge
(sitting allowance).

Mnamo tarehe 23/11/2015, mbunge wa Singida Magharibi (CCM) Mh. Elibariki Imanuel Kingu alimwandikia barua Katibu wa Bunge akieleza msimamo wake wa kukataa kulipwa posho ya kitako ya Bunge (sitting allowance) katika kipindi chote cha miaka mitano (2015 - 2020). Huyu anakuwa ni mbunge wa pili baada ya Mh. Zitto Kabwe kutoka hadharani na kukataa posho ambazo msingi wake ni unyonyaji wa wanyonge na ubadhirifu wa kodi za wananchi.

Jukwaa linapenda kumpongeza Mh. Kingu Mbunge kwa ujasiri wake na Uzalendo kwa Taifa lake, uliomfanya kuunga mkono juhudi za Mh. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa vitendo.
Jukwaa linatambua ya kwamba, mapambano ambayo Mh. Kingu Mbunge ameyaanzisha ni makubwa, magumu na yanahitaji kuungwa mkono na watanzania wote wanaoipenda nchi yao bila kujali itikadi za vyama. Tunafahamu, wapo baadhi ya wabunge wabinafsi na wasio na huruma na wanyonge wa Taifa letu ambao hawajafurahishwa na hatua hii ya wabunge kama Zitto na Kingu ya kukataa posho ya kitako. Baadhi ya wabunge wameanza kumpigia simu na kumtumia jumbe (sms) za vitisho mh. Elibariki Kingu (MB) na wengine wakibeza kuwa anatafuta cheo.

Jukwaa linalaani hatua za wabunge hao wanaopinga nia njema ya Mh. Elibariki Kingu na Mh. Zitto Kabwe kwa uamuzi wao wa kukataa posho za kinyonyaji na hivyo basi, Jukwaa linawaomba wananchi wote majimboni, kuwataka wabunge wao waliowachagua kueleza misimamo yao hadharani juu ya kuunga mkono hatua ya kukataa posho kama njia ya kupunguza matumizi ya Serikali yasiyo ya lazima.

Jukwaa linafahamu ya kwamba, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ndiye mwenye mamlaka ya mwisho ya kuidhinisha masharti ya kazi za kibunge na stahiki wanazopaswa kulipwa katika kazi hiyo.

Kwa heshima na unyenyekevu mkubwa, tunamuomba na kumshauri Mh. Rais John Pombe Magufuli atakapokuwa anaidhinisha masharti na stahiki hizo, atusaidie kuifuta kabisa posho ya kitako ya wabunge (sitting allowance).

Aidha, Jukwaa linamuomba mh. Rais kuzipitia na kutoa agizo la kufutwa kwa posho zote zisizo za lazima zinazolipwa kwa watumishi wa umma wa kada mbalimbali yakiwemo mashirika ya umma.

Jukwaa letu linatoa wito kwa wabunge wote bila kujali vyama vyao, kuungana na Mh. Kingu(MB) na Mh. Zitto(MB) katika kukataa malipo ya posho ya kitako ili kupunguza mzigo mkubwa ambao Serikali inaubeba kuhudumia wabunge. Fedha hizi ni vyema zielekezwe katika kutatua kero za wananchi vijijini kama vile ukosefu wa maji, madawati, vitanda vya Hospitali n.k.

Tunasisitiza kwamba, Ubunge ni Utumishi,na wala sio Utukufu. Kazi ya Mbunge ni kuwawakilisha wananchi wake na si kuwanyonya. Tufike mahali kama Taifa tuwe na nidhamu ya matumizi ya kodi za wananchi na mgawanyo sawa wa keki ya Taifa. Kuendelea kulipana posho hizo ni ishara ya unyonyaji, dhuluma na kuongeza pengo kati ya wenye nacho na wasionacho nchini. Jambo hili linakuza chuki na hasira miongoni mwa wananchi wa hali ya kawaida dhidi ya viongozi wao na serikali kwa ujumla.

Tunawaahidi kuwa Jukwaa litaendeleza harakati (movement) na vuguvugu hili kwa kuanzia na Bunge kwasababu ndio wawakilishi wa wananchi. Tutaendelea kupaza sauti zetu ili wabunge wengi zaidi Wazalendo wajitokeze na kukataaa posho hizi. Tunajua kuwa wapo miongoni mwao wabunge wazalendo ambao wataguswa na wito huu na kuuunga mkono hadharani.

Aidha tutaendelea kuwasemea kwa wananchi wabunge ambao bado hawataki kukataa posho hizi bila kujali vyama vyao. Tunawaomba wananchi kote nchini kutuunga mkono katika harakati hizi ili tuweze kuokoa mabilioni ya shilingi yanayopotea kila Bunge linapokaa Dodoma kupitia posho ya kitako (sitting allowance).
Ahsanteni sana.

ALLY SALUM HAPI - MWENYEKITI (0714 193161
MTELA MWAMPAMBA - KATIBU (0755 178927)


Tuesday, November 24, 2015

MCHUJO WA DARASA LA PILI KUPITIA NECTA

BARAZA la Taifa la Mitihani (NECTA) limesema ili kutekeleza sera ya elimu ya mwaka 2014, watoto wataanza kukariri darasa kuanzia wakiwa darasa la pili.

Alisema hatua hiyo itachukuliwa endapo watashindwa mtihani wa kujipima ambao utaanza rasmi mwakani kwa wanafunzi wa ngazi hiyo ya elimu.

Katibu Mtendaji wa Necta, Dk. Charles Msonde, aliyasema hayo mwishoni mwa wiki alipozungumza na gazeti hili.

Alisema kufanyika kwa mitihani hiyo kunakwenda sambamba na kuipa hadhi mitihani ya kupima wanafunzi katikati ya masomo ya darasa la nne na kidato cha pili ambayo kwa sasa itakuwa chini ya baraza hilo tofauti na ilivyokuwa awali.

Dk. Msonde alisema kwa upande wa mitihani ya darasa la pili, matokeo ya mitihani hiyo itasaidia kuwatenga wanafunzi hao kwenye makundi matatu ambayo walimu watatakiwa kuyafanyia kazi kuhakikisha watoto hao wakiendelea na madarasa ya juu watafanya vizuri.

Alisema kwa kuwaandaa watoto kwa mitihani hiyo, anaamini mpaka wakiwa wanamaliza darasa la saba hakuna ambaye atakuwa hajapata stadi za kusoma na kuandika kama ilivyo kwa sasa ambako baadhi uhitimu elimu ya msingi wakiwa hawajui kusoma na kuandika.

“Kwa kuanza kuwapima wakiwa darasa la pili watakuwa wanaangalia kwenye stadi za kusoma, kuandika na kuhesabu huku mitihani mingine kama ile ya darasa la nne ikipandishwa hadhi na kuwa chini ya baraza.

“Tunaamini suala la watoo kumaliza darasa la saba baadhi wakiwa hawajui kusoma na kuandika litaisha,” alisema.

Alisema mipango ya sera hiyo ikikamilika, mtihani wa darasa la saba ambao hivi sasa ni wa kuhitimu elimu ya msingi, utakuwa wa kupima kama ulivyo ule wa darasa la nne kwa sababu elimu ya msingi mwisho itakuwa kidato cha nne.

“Siwezi kusema ni lini hili litaanza kwa sababu utekelezaji wa sera ni mchakato, lazima kwanza madarasa ya sekondari yaongezwe.

“Mitaala ibadilike kama hivi sasa ambavyo ya darasa la kwanza na la pili imebadilika na ndiyo kwanza tunaanza kuwapima wanafunzi kwa mtihani huo wa darasa la pili.

“Faida nyingine ya mtihani huo na ule wa darasa la nne ni kuhakikisha mpaka mtoto anafika darasa la saba, wale watakaopata alama 100 chini ya 250 ambao kwa sasa ndiyo ufaulu wawe wameongezeka,” alisema Dk. Msonde.

Alisema ili kuona namna bora ya kuanza kufanya mtihani huo mwakani, leo watoto wa darasa la pili kutoka shule 66 zilizo kwenye mikoa 11 watafanya mtihani huo ikiwa ni sehemu ya majaribio.

Alisema kwenye mikoa hiyo zimechaguliwa wilaya ambazo zimetoa shule moja ya kijijini, moja ya mjini na nyingine ya mchepuo wa Kiingereza.

Sunday, November 22, 2015

MH. JOHN MAGUFULI BAADA YA KULIZINDUA BUNGE.


Mh. John Pombe Magufuli  wakibadilishana mawazo na Rais Mstaafu Ali Hassan Mwinyi  baada ya kulihutubia Bunge la kumi na moja (11) na kulizindua Mjini Dodoma.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. John Pombe Magufuli (Kushoto)  Rais wa Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein, (Kulia) Rais Mstaafu Ali Hassan Mwinyi, baada ya kuhutubia Bunge la 11, Mjini Dodoma.
Mh,Dk. John Magufuli akimkabidhi cheti Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NMB Mama Ineke Bussemaker kwa mchango wao.

Mh. John Pombe Magufuli akimshukuru na kumkabidhi cheti mwakilishi wa Benki kwa mchango wao baada ya kulizindua rasmi Bunge la 11 Mjini Dodoma.

Friday, November 20, 2015

UZINDUZI RASMI WA BUNGE LA KUMI NA MOJA (11).


Mh,Dkt. John Pombe Joseph Magufuli rais wa Jamhuli ya Muungano wa Tanzania amelihutubia bunge kwa mara ya kwanza inchini, akisisitiza kuwa Bunge ni chombo muhimu, halipaswi kuwa chombo cha malumbano, kutukanana, kutoka nje, n.k. Katika hotuba ya Mh.Rais John Pombe Joseph Magufuli Amesema anachukizwa sana na vitendo vya rushwa na ufisadi, Pia kasisitiza kuwa atahakikisha safari zote za nje ya nchi zinadhibitiwa ili kuongeza mapato ya nchi.

HOTUBA YA MHESHIMIWA DK. JOHN POMBE MAGUFULI.

Thursday, November 19, 2015

KUAPISHWA KWA WAZIRI MKUU KATIKA VIWANJA VYA IKULU.

Mh.John Pombe Magufuli akimkabidhi hati ya kiapo Waziri Mkuu wa Tanzania Kassim Majaliwa Kassim baada ya uchaguzi Mkuu uliofanyika hivi karibuni.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.John Pombe Joseph Magufuli  katika picha na Makamo wa Rais Mama Samia Suluhu Hassan (Kulia) Waziri Mkuu wa Tanzania Kassim Majaliwa Kassim.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.John Magufuli katika picha ya pamoja na familia ya Waziri Mkuu wa Tanzania Kassim Majaliwa Kassim baada ya kuapishwa katika viwanja vya Ikulu Dodoma.

DK. TULIA ACKSON NAIBU SPIKA WA BUNGE LA TANZANIA.

Dk.Ackson Mwansasu Naibu Spika wa bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, akila kiapo baada ya kuchaguliwa na Wabunge Mjini Dodoma.



Thursday, November 5, 2015

RAIS DK. JOHN POMBE MAGUFULI AKIELEKEA IKULU.

Rais Dk. John Pombe Magufuli  akiwa na Mkewe Mama Janeth Magufuli akiwasili Ikulu mara baada ya Kuapishwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mh. Dk Ally Mohamed Shein rais wa Zanzibar wakibadilishana mawazo na  Uhuru Kenyata wakati wa hafla iliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli akisalimiana na Mke wa Raila Odinga, na Mama Janeth Magufuli akisalimiana na Raila Odinga katika Picha.
Dk.John Pombe Magufuli rais wa Jamhuri wa Mungano wa Tanzania katika picha ya Pamoja.

Posted By Emman W